Hazina-Ofisi ya Msajili wa Hazina Zanzibar

Serikali ya Mapinduzi Zanzibar

Ofisi ya Msajili wa Hazina Zanzibar

TAARIFA KWA UMMA

Ofisi ya Msajili wa Hazina Zanzibar, inapenda kuutangazia umma kuwa, Kampuni ya Uunganishaji na Usambazaji Maudhui Zanzibar (ZMUX) imefutwa rasmi kuanzia tarehe 22/09/2025. Ufutaji wa Kampuni hiyo umefanyika kwa kuzingatia masharti ya Sheria ya Makampuni, Nam. 15 ya 2013. Majukumu yote yaliyokuwa yakifanywa na Kampuni hiyo, yatafanywa na Shirika la Utangazaji Zanzibar (ZBC).

NAIBU GAVANA MSTAAFU WA BENKI KUU YA TANZANIA (BOT) AELEZEA KUHUSU UMUHIMU WA USIMAMIZI WA MASHIRIKA YA UMMA

Naibu Gavana Mstaafu wa Benki Kuu ya Tanzania (BOT), Bw. Juma Hassan Reli, akizungumza na waandishi wa habari kuelekea Wiki ya Mashirika ya Umma Zanzibar inayotarajiwa kufanyika kuanzia tarehe 11 hadi 15 Oktoba 2025 katika Viwanja vya Mapinduzi Square, Kisonge, ameeleza kuwa serikali inawekeza kwenye mashirika ya umma kwa madhumuni ya kupata mapato kupitia gawio na kodi. Amefafanua kuwa Ofisi ya Msajili wa Hazina Zanzibar imeanzishwa kwa lengo la kutekeleza malengo ya Serikali Kuu kwa kuhakikisha mashirika ya umma yanaendeshwa kwa ufanisi, uwazi, na tija. Bw. Reli amesema: “Ofisi ya Msajili wa Hazina inapaswa kuandaa mikataba kwa mashirika yote, na mashirika hayo ni lazima yafuate masharti ya mikataba hiyo ili kupimwa mwenendo na ufanisi wake.” Ameongeza kuwa jukumu la ofisi hiyo linahusisha: Aidha, ametoa wito kwa mashirika yasiyoleta faida kufanyiwa utafiti wa kina ili kubaini chanzo cha changamoto na kuweka mikakati sahihi ya maboresho. Mwisho, amesisitiza kuwa mashirika ya umma yanapaswa kuendeleza utamaduni wa kibiashara (corporate culture) ili kuongeza tija na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.

Serikali Yasisitiza Umuhimu wa Gawio la Mashirika ya Umma

Serikali Yasisitiza Umuhimu wa Gawio la Mashirika ya Umma Zanzibar – Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema itaendelea kuchukua jitihada mbalimbali kuhakikisha Taasisi na Mashirika ya Umma yanafanya vizuri katika ugawaji wa gawio ili kuchochea maendeleo ya nchi. Akizungumza katika hafla ya uwasilishaji wa Ripoti ya Tathmini ya Mikataba ya Kiutendaji kwa mwaka 2024/2025, iliyofanyika katika ukumbi wa ZURA, Maisara, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango, Dkt. Juma Malik Akil, alisema bado kuna baadhi ya Taasisi hazijafanya vizuri katika kugawa gawio, jambo linalochelewesha juhudi za Serikali katika kukuza uchumi. Aidha, aliipongeza Ofisi ya Msajili wa Hazina kwa usimamizi wake madhubuti, pamoja na kupongeza Mashirika ya Umma kwa utendaji wao unaochangia ukuaji wa uchumi wa Taifa. Hata hivyo, alisisitiza kuwa bado changamoto kubwa ipo kwenye eneo la gawio, kwani upatikanaji wa gawio bado hauridhishi. Alifafanua kuwa gawio kutoka Taasisi na Mashirika ya Umma lina mchango mkubwa katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo, ikiwemo miradi mikubwa inayotekelezwa kutokana na akiba ya Serikali kupitia mapato ya ndani. Vilevile alisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuchukua juhudi za kuelimisha Taasisi juu ya nafasi na jukumu la Ofisi ya Msajili wa Hazina katika kusimamia mashirika hayo. Kwa upande wake, Msajili wa Hazina Zanzibar, Ndg. Wahid Ibrahim Sanya, alisema ofisi yake ina jukumu la kusaini mikataba mbalimbali na Taasisi za Umma, ambayo hupaswa kuwasilishwa kwa ripoti za utekelezaji ili kufanyiwa tathmini. Aliongeza kuwa changamoto kubwa bado ni uelewa mdogo wa baadhi ya Taasisi kuhusu utekelezaji wa majukumu yao ya kisheria na kiutendaji. Akiwasilisha ripoti ya tathmini ya mwaka 2024/2025, Mkuu wa Idara ya Mitaji ya Umma na Uwekezaji, Ndg. Ramia Mohammed Ramia, alisema Mashirika ya Umma yameonyesha maendeleo katika maeneo mbalimbali: Hata hivyo, ripoti imebainisha changamoto kadhaa ikiwemo ukosefu wa mafunzo ya mara kwa mara, udhaifu katika ukusanyaji wa mapato na gharama kubwa za uendeshaji.

Msajili wa Hazina Zanzibar Aongoza Kikao Kazi na Ziara ya Ukaguzi wa Mali Kisiwani Pemba

Msajili wa Hazina Zanzibar, Ndugu Waheed Muhammad Ibrahim Sanya, ameongoza kikao kazi na wafanyakazi wa Ofisi ya Msajili wa Hazina – Pemba, kikao kilicholenga kuimarisha utendaji kazi bora, wenye tija na ufanisi katika taasisi hiyo. Akizungumza katika kikao hicho, Ndugu Sanya aliwahimiza watumishi kuendelea kujenga mshikamano, nidhamu na ubunifu katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku. Amesisitiza kuwa jukumu la Ofisi ya Msajili wa Hazina ni kuhakikisha mashirika ya umma yanaendeshwa kwa ufanisi na kutoa mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa Zanzibar. Aidha, amewataka watumishi kuongeza bidii katika kuwahudumia wananchi kwa weledi na uwajibikaji, ili kuimarisha imani ya umma kwa mashirika ya umma na taasisi zinazoratibiwa na Ofisi ya Msajili wa Hazina. Pamoja na hayo, Ndugu Sanya aliwahimiza wafanyakazi kutunza amani na utulivu katika kipindi hiki cha kuelekea Uchaguzi Mkuu mwezi Oktoba 2025, sambamba na kushiriki kikamilifu katika zoezi la upigaji kura, ili kuendelea kuimarisha demokrasia na mshikamano wa kitaifa. Katika ziara yake kisiwani Pemba, Msajili wa Hazina Zanzibar pia alitembelea Msitu wa Ngezi, ambapo alikagua mali za serikali zilizopo eneo hilo, na kuangalia mali zinazotakiwa kuondoshwa ili kupisha ujenzi wa barabara. Ziara hiyo imelenga kuhakikisha rasilimali za serikali zinasimamiwa ipasavyo sambamba na kusaidia utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Kikao kazi na ziara hiyo vimekuwa fursa muhimu kwa Ofisi ya Msajili wa Hazina Zanzibar kuimarisha ufanisi wa utendaji wake, sambamba na kuweka mikakati madhubuti ya kulinda na kusimamia mali za serikali kwa manufaa ya taifa.

Katibu Mtendaji wa Kamisheni ya Utumishi wa Umma akabidhi Muundo wa Utumishi kwa Ofisi ya Msajili wa Hazina Zanzibar

Katibu Mtendaji wa Kamisheni ya Utumishi wa Umma Zanzibar, Bwana Kubingwa Mashaka Simba, amesisitiza umuhimu wa kutumia muundo wa utumishi ipasavyo katika kuboresha maslahi ya watumishi wa umma. Kauli hiyo aliitoa katika hafla ya kukabidhi muundo wa utumishi kwa Ofisi ya Msajili wa Hazina Zanzibar. Akizungumza katika hafla hiyo, Ndugu Simba alisema kuwa muundo wa utumishi ni nyenzo muhimu ya kuimarisha haki na maslahi ya watumishi, hivyo haupaswi kuwekwa kwenye makabati bali unapaswa kufanyiwa kazi kwa vitendo. Alisisitiza kuwa ni jukumu la watendaji kuhakikisha watumishi wanapatiwa elimu kuhusu utekelezaji wa majukumu yao kwa mujibu wa muundo huo, jambo ambalo litasaidia kuongeza ufanisi na uwajibikaji. Aidha, alieleza kuwa upimaji wa watumishi na upandishaji wa madaraja unatakiwa kufanyika kwa haki, kwa kuzingatia sifa na utendaji wa kila mmoja. “Watumishi lazima wapimwe na kupandishwa madaraja kwa mujibu wa stahiki zao, na ni wale wanaostahili pekee ndio watakaopata fursa hiyo,” alisema. Katibu Mtendaji huyo pia alihimiza watendaji wa taasisi kujua na kuelewa vizuri scheme of service, akibainisha kuwa Kamisheni ipo tayari kutoa ushirikiano na elimu kuhusu muundo uliopitishwa, ili kuhakikisha unatekelezwa kwa ufanisi na kwa manufaa ya watumishi pamoja na taasisi kwa ujumla. Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Rasilimali watu, Utawala na Mipango wa Ofisi ya Msajili wa Hazina Zanzibar, Bwana Makunga Ali Mzee alisema, kupitishwa kwa muundo huo kutapelekea wafanyakazi kutimiza majukumu yao inavyotakiwa, hali ambayo itapelekea ufanisi katika taasisi. Aidha kwa upande mwengine ameishukuru kamisheni kwa kukamilisha na kukabidhi muundo huo kwa wakati.